Ijumaa, 11 Aprili 2014

ULIMPOKEA ROHO MTAKATIFU ULIPOAMINI?


(Mtendo 19:1–3)
“Ikiwa Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu alifika Efeso, akakutana na Wanafunzi kadhaa wa kadha huko akawauliza Je, mlimpokea Roho Mtakatifu mlipo amini? Wakajibu la, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia. Akawauliza basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema kwa ubatizo wa Yohana.”
Aina gani ya Injili Paulo alihubiri? Alihubiri Injili ya ubatizo wa Yesu na damu yake. Matendo 19:1-2 inasema “Ikiwa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo akiisha kupita kati ya nchi za juu akafika Efeso, akakutana na Wanafunzi kadhaa wa kadha huko akawauliza, Je, mlimpokea Roho Mtakatifu mlipoamini?”
Hata hivyo watu hawa walikuwa wamekwisha mwamini Yesu huku wakiwa wameweka kando maana ya ubatizo wa Yesu. Hawakujua juu ya Injili njema ambayo hupelekea kumpokea Roho Mtakatifu ndani. Na hii kupelekea Paulo kuuliza “Je, mlimpokea Roho Mtakatifu mlipoamini?” lilikuwa swali geni kwa baadhi ya wafuasi. Watu wengine wangeliweza kuuliza “Je, una mwamini Yesu?” Lakini Paulo aliuliza swali katika njia isiyokuwa ya kawaida ili kwamba waweze kumpokea Roho Mtakatifu, ndani yao kwa kufanya upya imani zao katika Injili njema. Huduma ya Paulo ilikuwa ni kuhubiri Injili njema ya ubatizo wa Yesu kwa Yohana Mbatizaji. 
Hebu tuone ushuhuda wa Mitume katika Injili ya ubatizo. Kwanza Paulo alishuhudia “Hasha sisi tulioifia dhambi tutaishije tena katika dhambi? Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti yake?” (Warumi 6:2-3). “Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo” (Wagalatia 3:27).
 Mtume Petro naye pia alishuhudia Injili ya ubatizo wa Yesu katika 1 Petro 3:21–22 akisema “Mfano wa mambo hayo ni ubatizo, unawaokoa ninyi pia siku hizi (siyo kuweka mbali uchafu wa mwili, bali jibu la dhamira safi mbele za Mungu) kwa kufufuka kwake Yesu Kristo. Naye yupo mkono wa kuume wa Mungu amekwenda zake mbinguni, malaika na enzi na nguvu zikiisha kutiishwa chini yake.”
Mtume Yohana pia alishuhudia hii Injili njema katika 1 Yohana 5:5-9 “Mwenye kuushinda ulimwenguni ni nani isipokuwa ni yeye aaminiye ya kwamba Yesu ni mwana wa Mungu? Huyu ndiye aliye kuja kwa maji na damu. Naye Roho ndiye ashuhudiaye kwa sababu Roho ndiye kweli. Kwa maana wako watatu washuhudiao mbinguni Baba na Neno na Roho Mtakatifu na watatu hawa ni umoja. Kisha wako watatu washuhudiao duniani, Roho na maji na damu na watatu hawa hupatana kwa habari moja”.
Yohana Mbatizaji alichukua nafasi muhimu, katika kukamilisha Injili njema. Biblia inazungumzia yafuatayo juu ya Yohana Mbatizaji katika Malaki 3:1-3 na Mathayo 11:10-11.
Yohana Mbatizaji alikuwa mwakilishi wa wanadamu na alikuwa ni nabii Eliya ajaye kama alivyoandikwa katika Agano la Kale. Katika Agano la Kale, sadaka ya dhambi ilichinjwa ili kumwaga damu baada ya kubeba dhambi za mtu kwa tendo la kuwekewa mikono. Katika Agano Jipya, hata hivyo Yesu ndiye aliyesimama kama sadaka ya dhambi kwa kubeba dhambi ya ulimwengu kwa njia ya ubatizo na kifo chake Msalabani kulipa mshahara wa dhambi. Ubatizo wa Yesu kwa Yohana Mbatizaji pale Yordani ndiyo uliokoa wanadamu wote.
Mungu alipanga aina mbili za matukio ili kuweza kuwaokoa wanadamu tokana na dhambi zao na kuweza kutimiza haki yote. Tukio la kwanza lilikuwa ni kumfanya Yesu aje ulimwenguni kupitia mwili wa mwanamwali Bikira Mariam, na kuwezesha abatizwe na kusulubiwa ili kuondoa dhambi za ulimwengu. Tukio la pili ni kuwepo kwa Yohana Mbatizaji duniani kupitia Elizabeti mama yake. Mungu alisababisha matukio haya mawili yatokee ili wanadamu waweze kuokolewa kwa dhambi zao zote. 
Hii ni kazi ambayo Mungu aliipanga katika utatu. Mungu alimtuma Yohana Mbatizaji ulimwenguni miezi sita kabla ya Yesu, ndipo akatumwa Yesu Kristo mwokozi wa wanadamu hapa duniani kuwaweka huru wanadamu tokana na hukumu ya dhambi zao.
Yesu alishuhudia juu ya Yohana Mbatizaji katika Mathayo 11:9 “Lakini kwa nini mlitoka? Ni kuona Nabii? Naam, nawaambia na aliye mkuu zaidi ya Nabii”. Zaidi ya yote, pale Yohana Mbatizaji aliyemtwika dhambi zote za ulimwengu Yesu, alipo mwona tena siku aliyofuata yeye mwenyewe alishuhudia kwa kusema “Tazama! mwana kondoo aichukuaye dhambi ya ulimwengu” (Yohana 1:29).
Biblia ina taarifa nyingi za Yohana, aliye mbatiza Yesu na inatupasa kupekuwa na kutafuta ili kuweza kuwa na ufahamu mzuri juu yake. Yohana Mbatizaji alikuja ulimwenguni kabla ya
Yesu jukumu lake likiwa kutimiza Injili njema ambayo ndiyo mpango wa Mungu. Biblia inasema kwamba Yesu alikubali dhambi zote za ulimwengu juu yake toka kwaYohana, naye Yohana alimtwika dhambi hizo juu yake ili kutimiza mapenzi ya Mungu.
Tunamwita kuwa ni Yohana Mbatizaji kwa sababu alimbatiza Yesu. Ubatizo wa Yesu una maana gani? Neno “ubatizo” linamaanisha “kuoshwa” kwa kuwa dhambi zote zimekwisha kutwikwa juu ya Yesu kwa kupitia ubatizo wake, hivyo basi zimekwisha kuoshwa. Ubatizo wa Yesu una maana sawa na tendo la “kuwekea mikono” ambalo ile sadaka ya dhambi ilipokea katika Agano la Kale. Maana ya kiroho ya tendo la ubatizo ni “kutwika, kuoshwa au kuzikwa”. Ubatizo wa Yesu kwa Yohana ulikuwa ni tendo la ukombozi katika kuondoa dhambi zote za watu wa ulimwengu.
Ubatizo wa Yesu unaumuhimu sawa kama ilivyo tendo la kuwekea mikono, ambapo ni njia ya kutwika dhambi juu ya sadaka ya dhambi katika Agano la Kale. Kwa maneno mengine,
watu wa Israeli walitwika dhambi zao za mwaka mzima juu ya sadaka ya dhambi katika siku ya Upatanisho kwa kupitia tendo la kuwekea mikono ya kuhani mkuu. Sadaka hii katika Agano la Kale ilikuwa na dhambi sawa na ubatizo wa Yesu na kifo chake msalabani.
Mungu aliiteuwa siku ya Upatanisho kuwa ni muda wa kuondoa dhambi za wana wa Israeli. Katika siku ya kumi ya mwezi wa saba, kuhani mkuu alitwika dhambi za mwaka za watu wake juu ya kichwa cha sadaka ya dhambi kwa kuwekea mikono juu ya sadaka kwa upatanisho wa dhambi za watu. Na huu ndio mpangilio wa utoaji wa sadaka ambao Mungu aliuweka. Ilikuwa ndio njia pekee katika kutwika dhambi za watu juu ya sadaka ya dhambi na alifanya hivyo kwa tendo la kuwekea mikono ambalo ndiyo sheria ya milele Mungu aliyoweka.
“Na Haruni ataweka mikono yake miwili juu ya kichwa cha yule mbuzi aliye hai, na kuungama juu yake uovu wote wa wana wa Israeli na makosa yao, naam dhambi zao zote, naye
ataziweka juu ya kichwa chake yule mbuzi kisha atampeleka aende jangwani kwa mkono wa mtu aliye tayari na yule mbuzi atachukua juu yake uovu wao wote, mpaka nchi isiyo watu, naye atamwacha mbuzi jangwani” (Walawi 16:21-22).
Katika Agano la Kale, mwenye dhambi aliweka mikono juu ya kichwa cha sadaka ya dhambi na kutwika dhambi zake juu yake ili aweze kusamehewa. Na siku ya Upatanisho Haruni Kuhani Mkuu akiwa mwakilishi wa Waisrael wote, aliweka mikono yake juu ya kichwa cha sadaka ya dhambi ili kutwikwa sadaka hiyo dhambi zote za Waisraeli. Ndipo sadaka hiyo huchinjwa baada ya kubeba dhambi hizo.
Tendo hilo linamaana sawa ya kiroho kwa ubatizo (“Baptisma” ni Kigiriki, maana yake “kusafisha kuzikwa kutwikwa”) ambapo Yesu aliupokea toka kwa Yohana katika Agano Jipya. Kama alivyokuwa Kuhani Mkuu katika Agano la Kale alipoweka mikono yake juu ya sadaka ya dhambi ili kutwika dhambi za watu wa Israel, ndivyo hivyo dhambi zote za wanadamu zilitwikwa juu ya Yesu kupitia ubatizo wake na Yohana Mbatizaji. Ndivyo Yesu alivyokufa Msalabani katika kutupatanisha kwa dhambi zetu.
Hii ni Injili njema. Kama ilivyo Haruni kuhani Mkuu alivyotoa sadaka ya Upatanisho kwa niaba ya watu wa Israeli, Yohana Mbatizaji naye aliye uzao wa Kuhani Haruni alichukua jukumu hilo akiwa mwakilishi wa wanadamu juu yake Yesu. Mungu anaeleza mpango huu ulio mzuri wa ajabu kuhusiana na upendo wake katika Biblia kama ifuatavyo katika kitabu cha Zaburi 50:4-5 “Ataziita mbingu zilizo juu na Nchi pia wahukumu watu wake. Nikusanyieni wacha Mungu wangu waliofanya Agano nami kwa dhabihu” Amen, Haleluyah.
Historia ya Kanisa inasema kwamba hapakuwepo na Krismasi kwa karne mbili za mwanzo katika kuanzishwa kwake. Kanisa la Wakristo wa mwanzo pamoja na Mitume wa Yesu
waliadhimisha January 6 kama “Siku ya Ubatizo wa Yesu” tu, uliofanyika katika mto Yordani na Yohana Mbatizaji. Kwa nini waliweka msisitizo zaidi katika hilo, yaani ubatizo wa Yesu katika imani yao? Jibu lake ndilo ufunguo halisi wa Ukristo wadesturi ya Kitume.
Lakini natumaini hamtochanganya ubatizo wa waumini na ule ubatizo wa Yesu. Ubatizo wa waumini kama ilivyo siku hizi una maana tofauti na ule ubatizo wa Yesu alioupokea katika mto Yordani. Hivyo imetupasa sisi sote kupokea uwepo wa Roho Mtakatifu kwa kuamini ubatizo wa Yesu Kristo ambao alioupokea toka kwa Yohana na pia damu yake Msalabani. Ikiwa mtazamo wa Kanisa la kwanza uliweka kipaumbele juu ya hili kuwa ndilo Sakramenti muhimu, basi hili kwao waliona ndiyo egemeo la imani katika ubatizo wa Yesu na hivyo hata sisi leo hii tuchukulie ubatizo wa Yesu kwa Yohana kuwa ni sehemu isisyo epukika katika wokovu wetu.
Zaidi ya yote ni lazima tuufikie na kuikumbatia imani iliyo sahihi yenye ufahamu kamili ambayo husema kwamba Yesu ilimbidi asulubiwe kutokana na kubatizwa kwake na Yohana. Imetupasa
kuelewa kwamba Roho Mtakatifu huanza kuweka makazi ndani yetu pale tu tunapoamini ubatizo wa Yesu, kufa kwake msalabani na kufufuka kwake ili awe Mwokozi wetu. Ubatizo wa Yesu kwa Yohana na damu yake msalabani vyote vinamaana ya pakee katika Injili njema.
Njia ya tahadhari kwako katika kumpokea Roho Mtakatifu ni kuamini Injili njema ya ubatizo wa Yesu na damu yake. Ubatizo wa Yesu ulitakasa dhambi zote za wanadamu mara moja. Ulikuwa ni ubatizo wa ukombozi uliopelekea kwetu kumpokea Roho Mtakatifu. Kwa kuwa baadhi ya watu hawajagundua nguvu iliyomo katika ubatizo wa Yesu, basi wao huelewa hili kuwa ni kama sherehe ya kawaida.
Ubatizo wa Yesu hufanya sehemu muhimu katika Injili njema ambayo hutueleza namna ile Yesu alivyobeba dhambi zote za ulimwengu juu yake na hata kuikubali hukumu yake kwa kumwaga damu yake msalabani. Yeyote anayeamini maneno ya Injili hii iliyo njema hufanywa kuwa msharika wa Kanisa ambalo linamilikiwa na Bwana, na kufurahiya baraka ya Roho Mtakatifu.
Roho Mtakatifu ni karama toka kwa Mungu kwa wale wote waliokwisha kusamehewa dhambi zao. Kwa ubatizo wake, Yesu alikuwa “Mwanakondoo wa Mungu aichukuaye dhambi ya ulimwengu” kwa namna iliyotosha (Yohana 1:29). Katika Yohana 1:6-7 inasema “Palitokea mtu
ametumwa kutoka kwa Mungu jina lake Yohana. Huyo alikuja kwa ushuhuda ili ashuhudie ile nuru, wote wapate kuamini kwa yeye”. Ili kumwamini Yesu kuwa ni mwokozi wetu aliyechukua
dhambi zetu zote ni lazima tuelewe juu ya huduma ya Yohana na ushuhuda kama ilivyo andikwa katika Biblia. Ndipo tutaweza kumwamini Yesu Kristo kama Mwokozi wetu. Ili kuweza kumpokea Roho Mtakatifu pia tunahitajika kuwa na imani madhubuti iliyoshuhudiwa moyoni.
Hivyo kukamilisha Injili ya kweli iliyo njema ni lazima kuamini ubatizo wa Yesu kwa
Yohana na damu yake pale msalabani. Katika Mathayo 11:12 imeandikwa “Tangu siku za Yohana Mbatizaji hata sasa Ufalme wa mbinguni hupatikana kwa nguvu na wenye nguvu wauteka”. Kifungu hiki husemekana kuwa ndicho kifungu kigumu kueleweka kati ya vifungu kadha katika Biblia. Hata hivyo imetupasa kuwa makini kwa sehemu isemayo “Tangu siku za Yohana Mbatizaji”. Hakika hapa inatangaza kwamba huduma ya Yohana ilikuwa iimeunganika moja kwa moja na huduma ya Yesu kwa wokovu wetu.
Yesu anatuhitaji tuingie katika Ufalme kwa ujasiri wa imani kama ulivyo ujasiri wa mwenye nguvu. Tunatenda dhambi kila leo, sisi ni dhaifu lakini ameruhusu tuweze kuingia katika Ufalme wake kwa imani, kifua mbele bila ya kujali udhaifu wetu. Hivyo kifungu hiki kina maana kwamba watu wataweza kuuteka Ufalme wa mbingu kwa imani katika Injili njema isemayo kwamba Yesu amefuta dhambi zote za ulimwengu kwa kupitia ubatizo wake kwa Yohana na damu yake msalabani. Kwa maneno mengine ina maana kwamba mbingu inawezwa kutekwa kwa imani madhubuti katika Injili hii njema ya ubatizo wa Yesu na damu yake.
Ubatizo wa Yesu ndiyo uliobeba dhambi zote na imani yetu juu yake hatupa uhakika kwamba tutapokea uwepo wa Roho Mtakatifu ndani yetu. Lazima tuhubiri Injili hii kwa majirani zetu, ndugu zetu, wapendwa wetu na kwa yeyote Yule ulimwenguni. Lazima tuwe na imani katika Injili njema ambayo inasema kwamba dhambi zetu zote ulimwenguni zilitwikwa kwake Yesu kupitia ubatizo wake. Kwa kupitia imani yetu ndipo basi tutaweza kupokea tulizo la ukombozi na uwepo wa Roho Mtakatifu ndani. Kila mtu ataweza kuwa mwana wa Bwana ambamo ndani yake Roho Mtakatifu atakaa, kuwa moja kati ya kaka na dada kwa kuamini Injili njema ya maji na Roho. Ni lazima muwe na imani sawa katika Injili njema kama aliyokuwa nayo Paulo. Namshukuru Bwana kwa kutupa Injili njema na kumsifu yeye. Ameni.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni